I am targeted to change youth's mind set towards positivity.

I am targeted to change youth's mind set towards positivity.
I am targeted to change youth's mind set towards positivity

Sunday 3 December 2017

NIMEMPA MIMBA, WAZAZI WAKE WANATAKA NDOA NDANI YA WIKI MOJA,

Kama maandishi hayasomeki kwa mobile version, shusha mwishoni utakuta "View web version" click hapo.

Natambua fika hatari ya kujamiiana kabla ya ndoa na matokeo yake. Moja wapo ni mimba, na ikumbukwe hapa tatizo sio mimba bali ni mfumo wa kuipata/kusababisha na uwezo wa kuhudumia mimba yenyewe na mtoto atakayezaliwa. Hili nalitambua vizuri sana na nimekuwa nikiliongea na kuliandika kila uchwao, sio kwa kuhukumu hapana, hii ni kwasababu kuzaliwa ndani ya ndoa au nje ya ndoa hakufanyi azaliwe kiumbe tofauti, japo kuna hatari ya myumbo katika malezi na kumkosesha mtoto baadhi ya haki fulani za msingi au kukosa uhuru.

Katika hali isiyo ya kawaida nilijikuta nimempata msichana fulani na kufanya naye ngono, na kumpa mimba siku hiyo hiyo. Mimi  sikutambua kuwa nimempa mimba na yeye alisema kuwa hawezi kupata mimba. Basi baada ya muda fulani wazazi wake waliniita na kuniambia nimempa mimba mtoto wao na wanachotaka ni ndoa kabla mtoto hajazaliwa kwa maana hawataki mjukuu wa nje ya ndoa. Na ikiwezekana nimuoe ndani ya wiki moja.

Mungu wangu weee, presha ilinipanda, viungo vyote viliishiwa nguvu, nikawaza na kuwazua nitaishije na kumlea huyu binti, tena sina kazi na akaunti yangu benki inapumulia mashine hata elfu kumi hakuna. Nikawaza juu ya makazi na kugundua nina chumba kimoja tu nacho wanakaa wadogo zangu wawili wanaosoma tena ninawahudumia mimi mwenyewe na hawana sehemu ya kwenda. Rafiki yangu mmoja akaniambia ‘Nguki hapa komaa tu mzee baba, ndani ya wiki hii oa tu’.
Ukweli nilikuwa na hamu sana ya kuitwa baba, eh, niwe na mtoto. Lakini sasa njia niliyotumia ndiyo inayonipa majuto. Nikawa nawaza juu ya rafiki zangu na watu wa karibu, wataelewaje kuona ndoa imeibuka kama uyoga hakuna cha kuvalishana pete wala send off wala nini? Huku wazazi wa yule binti ndio kwanza hawataki kusikia chochote. Basi nikajikaza kisabuni hadi kwa baba yangu mlezi, akasema ‘hiyo changamoto umeizalisha mwenyewe na hakuna kukwepa. Mimi nitakuongezea hela kidogo kwaajili ya hizo harakati zako, kama utaongezea kwenye harusi sawa, kama ni kwemnye maisha utajua mwenyewe’ 


Kuna wakati mambo yanakaba hadi unajionea aibu wewe mwenyewe.


Kichwa kiliniuma sana, hadi nikahisi yule msichana ananidanganya. Nikampigia simu ili aje niliangalie tumbo vizuri kama linaonekana kuongezeka ukubwa. Alikuja na kunikuta nipo na rafiki zangu nimejiinamia kwa mawazo. Akafika pale akiwa ameniletea na mikate, nikamuaangalia kichovu na kumuuliza kama yuko serious kweli nilimpa mimba kwa tendo lile moja au ananipima tu akilia, akanisogelea kwa karibu, mamamamamamama weeeeeee, katumbo kamejaa mwanawane, yani hakuna ubishi. Akanishika kichwa changul kwa tabasamu na kuniambia kingereza ‘Nguki, do you think I am lying to you? This pregnancy is yours’. (Akiwa na maana nisidhani anadanganya, hiyo mimba ni yangu). Aliongea kwa kujiamini, bila wasiwasi huku akinishika kidevu changu kilichokauka kama mti mkavu kwa presha tangu nizipate hizi habari.

Kwakweli sijawahi pata maumivu ya kichwa na mawazo makali kama haya, nilitazama juu na kuona kama Mungu kaniacha, jeuri yangu ya kuwashauri vijana wenzangu ikayeyuka ghafla, nikiangalia wazazi wangu hawana uwezo wa kujitwisha hii changamoto. Nikajiuliza, nini kinafuata bado sikupata jibu. Nilijikuta nalowa jasho mchana na usiku sipati cha kufanya na wiki moja niliyopewa na wazazi wake yule binti niliye mtumbilize ndio hiyoooo inaisha.

Rafiki yangu akaniambia niende kwa wazazi wa yule binti kuwaambia nimeshindwa kutekeleza masharti yao na kama kuna lolote wanataka kufanya juu yangu kwakweli wafanye tu, maana sioni cha kufanya juu wala chini, zaidi najikuta nakonda tu ndani ya wiki moja. Basi yule jamaa yangu akanipakia kwenye pikipiki yake, haooooo hadi nyumbani kwa wazazi wa yule binti..
Kichwa kinazungukaaa kama mpira, lakini hakuna pa kutokea!


Tulimkuta mama yake akiwa nje, alipotuona tu, akamuita mumewe aliyekuwa ndani. La haulaaaaa, yule mzee alipotoka alinikata jicho hilo kwa muda katika tano bila kuongea chochote! Ohh Mungu wangu weeee, hofu ikanitanda, huku navuja jasho nikadondoka chini kama fulushi puuuuuu!, Wakati nahangaika kusimama  kwa kuishika mikono ya yule rafiki yangu, nikagundua nimeshikilia neti na nilikuwa nimezinduka kutoka kwenye ndoto yangu! Loooh, nilikuwa navuja jasho, nikainuka na kukaa, nikajikuta natamka kwa nguvu ‘Mungu, nini lakini jamani’. Asikwambie mtu, sijawahi ota ndoto yenye kashkash kama hii ya usiku wa kuamkia 25/11/2017. 
Nilipoamka nikawa nawaza hivi hizi presha ni katika ndoto, je ingekuwa live?


Narudia tatizo sio mimba bali mfumo. Aisee hizi presha sizitaki kabisaa,hii ni ndoto lakini imenipa picha nzima ya hali ambayo nitakutana nayo endapo nitajitoa ufahamu. Nakushauri na wewe kijana mwenzangu amini katika subira na jiwekee tu malengo, haya yote uyafaidi ndani ya ndoa. Narudia tena hapa hatunyoosheani vidole au kuhukumu, hapana, bali kama umewahi kukosea, basi fanya ukarabati mkubwa (Major rehabilitation) wa nafsi ili usikosee tena na kujiwekea nafasi nzuri ya kuwa mlezi bora wa familia.KUSUBIRI INAWEZEKANA, ANZA SASA.


Kitabu changu Kipya


Katika kujifunza pia nakukaribisha uniunge mkono kwa kununua kitabu nilichokiandika (DHAMIRI NA UTASHI VIMETEKWA) ambacho ndani nimeeleza mambo mengi yahusuyo mahusiano, upendo, subira, kuweka malengo, na malezi. Nimekielekeza kwa vijana, lakini pia wazazi na walezi kitawafaa sana ili kuongea na watoto/vijana wao. Ili kukipata waweza nitafuta kwa namba zangu hapo chini. Lakini pia kinapatikana  Dar es Salaam (Doloka Investment Company Ltd Millenium Towers Makumbusho-0655 266 993 na Pia Kijichi-0686 971 623), Morogoro kinapatikana chuoni Sua (nipigie nikuunganishe na wanaokiuza), Kinapatikana pia Fransalian Bookshop-Kola Morogoro na Iringa ofisi za UCE Tanzania, Kihesa-Kichangani.Karibu sana ujifunze.

Eng Herman Nguki
Email:ngukiherman@ymail.com
Instagram: eng.ngukiwamalekela

Phone #: 0763 639 101/ 0679 639 101
Asante kwa kusoma katika blog hii.Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com