I am targeted to change youth's mind set towards positivity.

I am targeted to change youth's mind set towards positivity.
I am targeted to change youth's mind set towards positivity

Sunday 20 August 2017

SABABU KUU MBILI ZA KUPENDA

Busara inatakiwa sana kuelewa mantiki ya upendo kwa mtu

Suala la kupenda ni suala mtambuka ambalo wakati fulani watu hutumia nguvu nyingi kujitahidi kutetea mantiki yake na kujikuta wanaishia kuongea uongo au kuharibu uhalisia. Kwa kawaida mtu akiulizwa sababu za kumpenda mtu fulani, anaweza kutoa majibu haya au yenye mlengo huu:

  • Kwasababu nayeye ananipenda
  • Kwasababu ni mzuri (mrembo/ handsome)
  • Kwasababu amewahi kunisaidia nilipokuwa na shida
  • Kwasababu anaonekana atakuja kuwa baba/mama bora wa familia
  • Kwasababu ana akili sana darasani
  • Kwasababu anaonekana mpambanaji sana na anajituma
  • Kwasababu ana pesa nyingi sana, nikiwa naye siwezi pata shida
  • Kwasababu ni mpole na sio mlevi
  • Na mengine mengi


Sawa lakini yote hayo huenda ukawa ni ushawishi wa kupenda, lakini sio sababu ya kupenda. Kuna utofauti kati ya sababu ya kufanya kitu na ushawishi wa kufanya kitu. Sababu ni hamu na muwako wa ndani wa kufanya kitu, kumbe ushawishi ni kitu ambacho kinakufanya uamini kuwa utakuwa salama baada ya kufanya hicho kitu.
Mfano rahisi. Tamaa ni sababu ya kufanya ngono, lakini matumizi ya kondomu ni kishawishi cha kufanya ngono. Nadhani hapo umeelewa utofauti kati ya haya maneno mawili
Upendo ni lazima uwafaidie wote , na sio wa kibinafsi


Sasa sababu mbili kuu za kupenda ni hizi hapa:
  1. Ni hitaji la kila kiumbe hai
  2. Ni amri


KUPENDA KAMA HITAJI
Hili lipo wazi  kabisa, hakuna mtu asiyetaka kupendwa. Ndio hata mimi najisikia raha sana ninapogundua mtu fulani ananipenda. Kuanzia wazazi wangu, walezi wangu, wanafamilia, walimu na marafiki wa jinsia na kada zote. Kupendwa kunaleta msisimko wa aina yake na kukufanya uone uko ‘PROTECTED AND SECURED’  kwa sala za wanaokupenda na unaamini muda wowote ukiwashirikisha jambo wataitikia kwa muitikio chanya (positive response). Ni wazi mtu kama hakupendi hawezi kukuombea kwa Mungu mafanikio au hata afya njema. Fuaraha yake ni kuona unaishi kwa wasiwasi, mateso na maumivu au hata kutoweka kabisa. 

Hili halipo tu kwa binadamu, hata mifugo yako nyumbani, ikigundua unaipenda na kuihudumia, utaona kabisa inaonesha ishara ya kukufurahia na kila mara urudipo nyumbani lazima irukeruke miguuni pako. Najaribu kuwaza hata miti na maua ya nyumbani ambayo kila siku unayatunza, kuyamwagilia na kuyawekea mbolea, laiti yangekuwa na mdomo yangezungumza na kukubali (appreciate) upendo unaoonesha kwayo.
Ukifahamu hilo ndivyo inavyokuwa upande wa pili, kama unafurahia kupendwa basi na wewe kuwapenda wengine ni lazima, kwa maana wanahitaji hilo, na ni la kudumu.  Watu wanapata vidonda vya tumbo, presha na msongo wa mawazo na wengine afya zao kuzorota mara wakigundua hawapendwi au kutothaminika na watu walio karibuu nao. Ulishajiuliza siku mtu wako wa karibu akikutamkia ‘SIKUPENDI WEWE, YANI NATAMANI KAMA NISINGEIONA HIYO SURA YAKO’ utajisikiaje? Wakati fulani sio lazima mtu atamke, lakini mambo yake tu yanatoa picha kuwa hampendi mtu fulani.


Na wapo wengine wako katikati (neutral), yani yeye anajipenda yeye mwenyewe tu, mweee jamani, sasa si uende baharini huko utafute kisiwa ukae huko peke yako? Kama unaona hilo ni gumu, tafsiri yake ni kwamba tunahitajiana na kutegemeana. Unapotembea tu huko nje na kuona watu wamefurahi, hawana huzuni, hiyo ni dawa pia na fundisho kuwa huwezi kujifurahisha mwenyewe, ili mtu ucheke, lazima uchekeshwe na mtu mwingine, kama sio mko uso kwa uso basi hata kwa message tu mnazochati. Kwa lugha rahisi tujifunze kuwapenda watu pasi na kujali matabaka ya aina fulani

Angalizo: Kwakuwa kupendwa ni hitaji, wapo wanaotumia mgongo wa uhitaji huo na kupeleka kwa watu upendo nusu kilo,  mateso na maumivu kilo hamsini. Hiyo ni dhambi kwa maana mpokeaji alijiandaa kuwa aliyemuendea ni mtu mwema anayefahamu kuwa kupenda na kupendwa ni lazima kati ya mtu na mtu au jamii na jamii.
Ni rahisi kutamka neno NAKUPENDA, lakini ukweli tunao wenyewe mioyoni


KUPENDA KAMA AMRI
Upendo ni amri ya Mungu. Nimejaribu kufuatilia mawaidha ya dini zote, mathalani Wakristu na Waislamu, wote wameagizwa kupenda, na kwamba kama wasipowapenda binadamu wenzao basi na Mungu hatawapenda wao. Ahaaaaa, kumbe kama hujui kupenda basi huwezi kuambatana na baraka za Mungu. Upendo hauhitaji pesa au mazingira maalumu au kuwekewa mikakati kama bajeti ya kujenga reli ya standard gauge, la hasha! Ukitambua tu kuwa ni amri ya Mungu , basi ni kujifunza tu kuwa ni sehemu ya maisha yako.


Upendo unaozungumzwa hapa hauna masharti, vionjo tatanishi na vitenzi vichokozi vyenye mlengo wa kumuinua shetani. Kwani hujawahi kuona mtu anasema ‘nilimuua mume wangu ili niishi kwa amani na mtu NINAYEMPENDA’, Sasa huo ni upendo? Hapana, ni ushetani kwa maana huyu wasasa akibadilika kidogo tu na akaja anayejali zaidi, basi atamuua na huyu ili afurahie na huyo mwingine. Hivyo ndugu zangu ni bora tukafahamu jambo hili kinagaubaga ili tusichanganye mambo na kudhani kupenda ni hiari, hapana. KUPENDA NI LAZIMA, lakini KUHUSIANA NI HIARI YA MTU. Kumpenda mtu sio lazima muhusiane, au kuzoeana bila mipaka, hapana, tupendane, tushirikiane, lakini mipaka na heshima iwepo ili kulinda utu wa mtu, misingi ya kijinsia, utamaduni na uhuru wa kuamua juu ya msatakabali wa maisha ya baadaye ya mtu binafsi. Kama una swali, hoja au maoni, kuwa huru hapo chini eneo la comments. NAWAPENDA WOTE

Eng Nguki Herman. M
Instagram: @eng.ngukiwamalekela
Phone: 0763 639 101/ 0679 639 101
Asante kwa kupitia na kusoma haya.Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com

Thursday 17 August 2017

ASIYETAMBUA NAFASI YA BIKRA MARIA KTK UKOMBOZI SIO MKRISTU!

Bikira Maria mama wa Mungu, Utuombee

Tumsifu Yesu Kristu/Bwana Yesu asifiwe/Shaloom.  Nakusalimu ndugu yangu katika Kristu Yesu mwana wa Mungu ambaye kupitia yeye tumekuwa wamoja kwa namna fulani. Naomba kukuondoa hofu kama utakuwa ni mmoja kati ya waliokwanzika na kichwa cha somo hili, kwa maana utakuwa umejikwaza mwenyewe kwa kujikataa au kuenda kinyume na ukweli. Kuwa mpole na usome taratibu maelezo yangu , na kama una hoja au kitu cha kupinga basi utatiririka hapo chini kwenye eneo la ku-comment, namimi bila hiyana nitakuja kukuweka sawa.

KWANI BIKIRA MARIA NI NANI?
Biblia takatifu imedadavua na kukakavua kinagaubaga juu ya mama Maria, fungua  kwa muda wako Injili ya Luka kuanzia sura ya kwanza aya ya 26 na kuendelea. Kwa kifupi Bikira Maria ni mwanamke safi, aliyeteuliwa na Mungu ili kupitisha nafsi yake ya pili (Yesu Mwokozi), yani kuwa mzazi wa Yesu Kristu Mungu kweli na mtu kweli. Alijazwa neema, kutunzwa na kulindwa ili abaki bila doa hata kumbeba mkombozi tumboni mwake. 

  Kama hiyo haitoshi, hakuishia kumzaa tu mtoto Yesu na kumuacha akapambane na hali yake, NOOOOOOO, aliendelea kumlinda, kumtunza (kumbuka pale walipokuwa wanamtafuta roho juujuu Luka 2:43-52), usisahau pale walipomkimbiza mtoto kwenda Misri  ili asiuawe na Herode (Mathayo 2:12-21) mara anaambiwa maneno ya kumchoma moyo juu ya huyu mtoto (Luka 2:35) bado akaendelea naye hata katika safari ya mateso hadi msalabani (Yohana 19:26-27)

Mafundisho makuu manne (DOGMA) kuhusu Mama Maria
  1. Maria Mama wa Mungu
  2. Maria Bikira Daima
  3. Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili
  4. Maria Mpalizwa Mbinguni


Leo sitaki kuanza kuyachambua hayo mnne kwa maana kila moja tu laweza kuwa mada ya kujaza kurasa nyingi. Angalau moja tu, kama huamini kuwa Bikira Maria makazi yake ni Mbinguni , nenda kasome Ufunuo sura ya 12 kuanzia aya ya kwanza na kuendelea na uje na jina la mwanamke anayezungumzwa hapo.

Wapo baadhi ya watu bila aibu mbele za Mungu wanasema kwao Maria sio kitu, wao wanamuangalia Kristu pekee kwa maana hakukuwa na ulazima wa Mungu kumtumia Maria na angeweza kumtumia hata mwanamke yoyote. Hivyo Maria alishamaliza kazi yake na hana umhimu wowote kwao. Hii ni kufuru mbele za Mungu ambaye ndiye aliyemtakatifuza huyu mama ili awe chombo kitakatifu kilichombeba mkombozi. Tatizo ni mafundisho yaliyokaa kimfumo wa kuoteshwa na vionjo vyenye ukakasi na kuwarithisha watoto uvuguvugu kisa tu hutaki kutafakari.

Maswali machache ya kujiuliza
  1. Kama unaamini kuwa Yesu Kristu ni Mungu kweli, nafsi ya pili ya Mungu Baba aliyeshikamana pamoja na Roho Mtakatifu bila kutengana, mbona unapata kigugumizi kusema Maria ni Mama wa Mungu (Yesu)?
  2. Kama Maria alishamaliza kazi yake ya kumzaa Yesu,na sasa hana umhimu wowote, basi na Yesu alishamaliza kazi yake na sasa hana umhimu wowote?
  3. Kama hakukukuwa na upekee wa Maria na Mungu angeweza kumtumia mwanamke yoyote, kumbe pia hapakuwa na ulazima wa Mungu kumtumia Yesu kutukomboa na angemtumia mtu yoyote?


Najaribu kuwaza kwa sauti hasa ninapoona wengi wakifanya mrejeo kwa wateule wengi wa zamani katika Biblia kama Musa, Elia, Daudi na wengine, lakini likija suala la Bikira Maria mhhhh, hapo wanaona mapichapicha. Wengi ukiwadodosa wanajing’atang’ata tu na kuishia kusema yeye anaangalia wokovu tu ulioletwa na Yesu, hataki kujua kuwa huyu Yesu hadi kutujia kuna watu ambao Mungu aliamua kushirikiana nao kujimwilisha (incarnation) ili tumuone na kumpokea katika umbo la kibinadamu. Kazi ya Bikira Maria ilitabiriwa tangu agano la kale huko Isaya  7:14 na kuelezewa matokeo yake katika agano jipya.

Angalau siku hizi kuna baadhi ya watu wa madhehebu yasiyo ya Kikatoliki wameanza kustuka na kujua kuwa walikuwa wanafanya makosa kutomheshimu mama wa Mkombozi wao hivyo kwa mbaliiiii wameanza kumtaja taja na kumheshimu, japo kwasababu ya kukosa msaada wa mafundisho au kuogopa wachungaji wao, basi wanashindwa kupata mang’amuzi ya hali ya juu na kujizolea neema kutokana na maombezi ya Mama huyu kwa mwanaye Yesu. Wapo ambao taratibu wameanza kusali Sala ya Salamu Maria na hata Rozali japo wanakuwa waoga kutokana na upande waliopo kutopigia chapuo sala hizi zenye nguvu ya kimungu ndani yake. Yeye mwenyewe kasema 'vizazi vyote tutamuita mbarikiwa' (Luka 1:48), sasa asijejua hili ni kizazi cha sayari gani?
Bikira Maria, Mama wa Amani, Utuombee


KUABUDU Vs KUHESHIMU.
Anayepaswa kuabudiwa ni mmoja tu (Kumbukumbu la Torati 5:7), naye ni Mungu muumba mbingu na nchi. Kuna watu pia wanapata ukakasi na kuwalishaa watoto wao matango poli kwa kusema wakatoliki wanamuabudu Bikira Maria, la hasha! Sio kweli, wao wanamuheshimu tu, tena heshima hiyo hatujakurupuka tu kumpa, bali ni Mungu kwanza ndiye aliyemuheshimu na kumkinga na doa la aina yoyote ili afanyike chombo cha kubeba nafsi yake kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Sasa jamani kama Mungu mwenyewe kamheshimu na kumpandisha hivi, sisi ni akina nani hata tumdharau? Ndio maana nimesema mtu asiyetambua nafasi ya Bikira Maria katika kuletwa kwa ukombozi huyo sio Mkristo bali anaigiza kuwa Mkristo.  

Bikira Maria ameshatokea mara kadhaa duniani hapa na ushahidi wa wazi kabisa upo. Maeneo kama Fatima, Lurdi Ufaransa, Kibeho Rwanda n.k yanatoa fundisho kwa dunia juu ya kumheshimu huyu mama. Hakuna mtu aliyewahi kupinga matokeo haya kwa maana ni matokeo ya wazi kabisa ambapo ni Mungu yule yule aliyemteua awe mama wa mwokozi anathibitisha kuwa uteule wake u hai hata leo huko mbinguni na duniani.
Bikira Maria ,kikao cha hekima, Utuombee

Kama unavyopata ujasiri wa kumwambia binadamu mwenzako akuombee kwa Mungu, sasa nakushauri utumie nafasi hii adimu kumwambia Mama Bikira Maria ambaye yuko Mbinguni uso kwa uso na Mungu akuombee kwa Mungu na mwanaye Yesu Kristu naye atafanya hivyo. Wewe omba kwa imani na matokeo utayaona.

TUOMBE:

Ee Mungu mwema, Baba wa Mataifa yote, kwa wema wako uliamua kumteua Mama Bikira Maria awe mama wa Mkombozi wetu Yesu Kristu, tunakuomba uturehemu na kutusamehe pale tunapokengeuka na kudharau heshima hiyo kubwa uliyompa mama huyu. Tena tunaomba msamaha na kwa mwanaye Yesu Kristu ambaye kabla ya kushuka duniani alikuwa kashikamana nawe kama nafsi yako, hivyo alishiriki kumteua mama Bikira Maria ili atusamehe na kutustahilisha baraka zako. Tena tunaomba msamaha na kwa Roho Mtakatifu ambaye mara kadhaa tumejigamba kujazwa naye kumbe ni vionjo vya kibinadamu na viini macho, na ndani mwetu tumejaa maasi hata kumdharau mama wa mkombozi. Nawe Maria Mtakatifu mama wa Mungu, utuombee kwa Mungu ili sala zetu ambazo mara kadhaa zinakwamishwa na maovu yetu ziweze kupokelewa, nasi kwa unyenyekevu tunaahidi kukuheshimu na kuthamini kazi yako ya kushirikiana na Mungu kutuletea Yesu, Bwana na Mwokozi wetu. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristu, anayeishi na kutawala  pamoja na Baba, Mungu daima na milele. Amina

Eng Herman Nguki.M
Email: ngukiherman@ymail.com
Phone: 0763 639 101/0679 639 101
Instagram : @eng.ngukiwamalekela
Asante kwa kusoma katika blog yangu.Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com