Monday, 11 September 2017

KUWA MAKINI NA WATU HAWA. NI HATARI

Masikio yako yachuje kila unaloambiwa kabla ya kuchukua hatua.

Leo ni siku ya kutafakari baadhi ya aina ya watu ambao tunatakiwa kuwa nao makini sana hasa wale wenye nafasi ya kuweza kubadilisha mawazo yako. Kuna kundi la watu huenda wapo kwako kama marafiki maalumu sana kama ambavyo kilatini wanaitwa familiaritas au confidential friendship kwa kingereza. Hawa ukiwashirikisha mipango yako, na ikatokea wakakupatia marekebisho au mapendekezo lazima kuna uwezekano wa zaidi ya 70% kuyakubali.

Sasa nikupe orodha ya baadhi ya watu ambao inabidi unatakiwa kujua hawafai kuwaamini na wanaweza kukupeleka porini na kukwamisha mipango yako:

01.  Mtu anayeona yeye ni bora kuliko wengine wote:
Hapa lazima tuwekane sawa tafadhari. Point hii hailengi kumfanya mtu ajione dhaifu, la hasha!. Hapa nalenga mtu ambaye katika mazungumzo yake yote hufanya marejeo ya udhaifu wa wengine ukilinganisha na uimara wake. Mfano ukiona mtu kwenye mazunumzo yake kauli kama ‘Usinifananishe mimi na fulani, mimi nina uwezo zaidi/ unapoteza muda kuwa na fulani, mimi ndio ninauwezo wa kukuhudumia/ umempendea nini yule? Ona mimi nina x,y,z ambazo yule hana uwezo wa kuwa nazo/ Mimi ni mzuri sana, siendani na wewe, au unaniona kama fulani, mimi ni msomi kuliko fulani, mimi nina akili kuliko fulani’ hazikosekani basi ujue mtu huyu kuna uwezekano mkubwa wa kukupoteza au kutokuwa na mchango chanya kwenye ushauri wake, na pia wengi ni waongo.

02.Mtu anayejihami bila sababu (Defensive people).
 Hii ni aina ya watu ambao wao huwa wanajitanguliza kuona wapo sahihi kabla hujaanza kuhoji utendaji wao. Kwa mfano ukiona mtu unamwambia; ‘hapo umekosea’ halafu yeye anajibu ; ‘unadhani nilifanya makusudi? Sasa unadhani kwa mazingira haya ningefanyeje? Hata ungekuwa wewe ungefanya hivihivi’. Mtu kama huyu kufanya marakebisho baada ya kukosea huwa ni mgumu sana. Unatakiwa kuwa naye makini sana, na kama ni mwanafamilia (mke/mume) itakuwa vyema ukimtambua kwenye kipengere hiki, vinginevyo unaweza kuwa unaumia moyo kila siku na wakati mwingine kukosa amani ndani ya moyo wako.

03.Mtu anayelazimisha wote kuamini njia yake ya mafanikio ndio pekee ya kufuata
Hapa ndio kwenye shida zaidi, na watoto wadogo ndio walio kwenye hatari kubwa sana ya kuambukizwa huu ugonjwa. Kwa mfano, wapo watu ambao wamefanikiwa nje ya mfumo wa taaluma, sio kwasababu waliamua tu kuelekea huko, bali kuna mazingira yaliwatoa kwenye taaluma na kujikuta wanafanikiwa kutumia vipaji binafsi au kusaidiwa na watu wa karibu walio na msingi bora kwa kifedha. Watu wa aina hii baadhi yao hujikuta wanawaweka njiapanda walio kwenye taaluma kwa kuwaambia kuwa wanapoteza muda huko na hawatafanikiwa, na afadhari wajiunge nao nje ya mfumo wa taaluma kitu ambacho ni hatari sana kwa maana sio kila mtu anaweza kufanya kila kitu katika mazingira yote. Wapo pia ambao kwasababu wamefanikiwa kwa njia ya taaluma, basi wanawavuruga vichwa wale wanaopambana nje ya taaluma na kujikuta hawaweki bidii huko waliko. Huu ni upotoshaji, acha kila mtu afuate njia ambayo Mungu amempangia, kikubwa iwe sahihi na yenye kukubalika. Watie moyo watu kule waliko, sio lazima wote uwalazimishe kufanya kama wewe, na mambo yakiwachachia huko, utaanza kuwacheka tena kwa kuwaambia wanazembea au hawakusikilizi vizuri.
Kazi kwako, utamsikiliza yupi na uache yupi
.
04. Mtu anayesifia uovu kama njia ya kawaida ya maisha.
Vijana wengi tupo kwenye huu mtego wa kushawishiana. Kwa mfano mtu anajisifia uhodari wake wa kuwa na mahusiano holela kwa siri, udanganyifu, wizi, matusi, kutoheshimu wazazi au walezi, unyanyasaji katika mahusiano au katika mazingira yoyote. Ukiona katika mazungumzo yake mtu haoni aibu kujisifia katika mambo haya huyo ni hatari katika mustakabali na ustawi wa jamii yoyote ile, na haaminiki kwa lolote kwa maana dhamiri yake imesheheni dumuzi na uso usio na huruma kwa wanaoteseka kwa matokeo ya maamuzi yake.

05. Mtu asiye na ratiba. 
Hora argentum’; ni msemo wa kilatini unaofanana na ule wa kiingereza ‘time is money’ ikiwa na maana muda ni pesa/mali. Mtu ambaye hana mpango mkakati wa kuhakikisha anafanya jambo fulani kwa muda fulani mambo yake kamwe hayawezi kwenda. Ukiona mtu yupo tayari kwenda mahali popote anapoambiwa aende kwa muda wowote huyo hana ratiba , hafahamu namna ya kufanya kwanza jambo la kwanza. Yaani kuna watu rafiki yake akimwambia waende mjini anakubali bila kuhoji anaenda kufanya nini na je lilikuwa kwenye ratiba yake? Wakiwa njiani akipigiwa simu na  rafiki yake mwingine kuwa waende porini anakubali, hehhh, jamani, yani ikifika jioni yuko hoi na hakuna hata moja la kujivunia alilofanya katika ratiba yake. Kiukweli mtu asiyejari muda mimi huwa hazipandi kabisa. Lazima tufahamu kuwa muda ni rasilimali ya kipekee ambayo ni kama haionekani (invisible resource) lakini ikipotea hairudi tena, hivyo mtu asiye na ratiba unatakiwa kuwa naye makini sana ili usije ungana naye kuelekea shimoni.

06. Mtu asiyetaka kurekebishwa/asiyefundishika.
 Hili ni kundi jingine ambalo unatakiwa kuwa nalo makini sana. Baadhi ya watu wakisikia maonyo, wao hukimbilia kusema ‘hili halinihusu’ , yani kila kitu kinachomgusa yeye anaona kina wahusu watu fulani na sio yeye. Na hata ukigundua ana udhaifu fulani na ukaanza kumuelekeza, anaona kama unamtuhumu na anaanza kukwepa na kuhakikisha hauendelei kuongea, hasa mambo yanayoonekana kuwa binafsi kama mahusiano, lakini ukweli ni kwamba siyo ya binafsi kwa maana madhara yake huenda hadi kwa jamii iayokuzunguka kwa namna moja ua nyingine hata kama sio moja kwa moja.


07. Mtu mwenye mafungamano na ushirikina.
Nikisema hivi mtu anadhani namzungumzia mshirikina wa moja kwa moja. Hapana, huko ni mbali sana, mimi nazungumzia mtu wa kawaida ambaye muda mwingi anawaza kulogwalogwa tu, story zake ni za wahirikina tu, anataka aishi kama jiwe, yaani hata akipata kakipele tu kutokana na baridi, basi anakosa usingizi na kusema kuna mtu amemloga. Anajichagulia mfumo wa uuguaji, yani anampangia Mungu kuwa anataka asiugue ghafla, maana ikitokea tu hivyo kwake yeye tuhuma zake ni kwa wachawi tu, anajisahau kuwa mwili ni kama maua ya miti, hata upepo ukipuliza, lazima utayumba kidogo. Watu wa aina hii mfumo wao wa kufanya maamuzi ni mbovu, kiufupi hata aina ya ushauri wanaotoa huwa sio wa kujiamini na wameweka rehani amani yao kwa mambo yanayofikirika ambayo hawana uhakika nayo. Epuka kuwarithisha watoto hofu ya aina hii kwa maana inawafanya hata wao kuwa washirikina indirectly. Kuna wakati hata madhehebu ya dini hunasa kwenye huu mtego kwa kwa kuwajaza hofu ya kuwaza mapichapicha yasiyo na mashiko kwa mfumo huu.


Kwa leo niishie na hizo tabia chache angalau tupate nafasi ya kutafakari. Kitu cha msingi ni kuwa makini sana unapokuwa karibu na watu wenye tabia hizo, na ikumbukwe wengi hujiona kama wapo sahihi na busara kubwa sana inahitajika wakati wa kuwaelekeza ili wabadilike au hata kupunguza madhara yake kwao binafsi au watu wanaowazunguka. Kama ukiwa na swali au maoni unakaribishwa hapo chini kwa sehemu ya comment. Tafakari njema!
Eng Nguki Herman. M
Instagram: @eng.ngukiwamalekela
Twitter: @engngukiherman

Asante kwa kusoma blog yangu.Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com

Sunday, 20 August 2017

SABABU KUU MBILI ZA KUPENDA

Busara inatakiwa sana kuelewa mantiki ya upendo kwa mtu

Suala la kupenda ni suala mtambuka ambalo wakati fulani watu hutumia nguvu nyingi kujitahidi kutetea mantiki yake na kujikuta wanaishia kuongea uongo au kuharibu uhalisia. Kwa kawaida mtu akiulizwa sababu za kumpenda mtu fulani, anaweza kutoa majibu haya au yenye mlengo huu:

  • Kwasababu nayeye ananipenda
  • Kwasababu ni mzuri (mrembo/ handsome)
  • Kwasababu amewahi kunisaidia nilipokuwa na shida
  • Kwasababu anaonekana atakuja kuwa baba/mama bora wa familia
  • Kwasababu ana akili sana darasani
  • Kwasababu anaonekana mpambanaji sana na anajituma
  • Kwasababu ana pesa nyingi sana, nikiwa naye siwezi pata shida
  • Kwasababu ni mpole na sio mlevi
  • Na mengine mengi


Sawa lakini yote hayo huenda ukawa ni ushawishi wa kupenda, lakini sio sababu ya kupenda. Kuna utofauti kati ya sababu ya kufanya kitu na ushawishi wa kufanya kitu. Sababu ni hamu na muwako wa ndani wa kufanya kitu, kumbe ushawishi ni kitu ambacho kinakufanya uamini kuwa utakuwa salama baada ya kufanya hicho kitu.
Mfano rahisi. Tamaa ni sababu ya kufanya ngono, lakini matumizi ya kondomu ni kishawishi cha kufanya ngono. Nadhani hapo umeelewa utofauti kati ya haya maneno mawili
Upendo ni lazima uwafaidie wote , na sio wa kibinafsi


Sasa sababu mbili kuu za kupenda ni hizi hapa:
  1. Ni hitaji la kila kiumbe hai
  2. Ni amri


KUPENDA KAMA HITAJI
Hili lipo wazi  kabisa, hakuna mtu asiyetaka kupendwa. Ndio hata mimi najisikia raha sana ninapogundua mtu fulani ananipenda. Kuanzia wazazi wangu, walezi wangu, wanafamilia, walimu na marafiki wa jinsia na kada zote. Kupendwa kunaleta msisimko wa aina yake na kukufanya uone uko ‘PROTECTED AND SECURED’  kwa sala za wanaokupenda na unaamini muda wowote ukiwashirikisha jambo wataitikia kwa muitikio chanya (positive response). Ni wazi mtu kama hakupendi hawezi kukuombea kwa Mungu mafanikio au hata afya njema. Fuaraha yake ni kuona unaishi kwa wasiwasi, mateso na maumivu au hata kutoweka kabisa. 

Hili halipo tu kwa binadamu, hata mifugo yako nyumbani, ikigundua unaipenda na kuihudumia, utaona kabisa inaonesha ishara ya kukufurahia na kila mara urudipo nyumbani lazima irukeruke miguuni pako. Najaribu kuwaza hata miti na maua ya nyumbani ambayo kila siku unayatunza, kuyamwagilia na kuyawekea mbolea, laiti yangekuwa na mdomo yangezungumza na kukubali (appreciate) upendo unaoonesha kwayo.
Ukifahamu hilo ndivyo inavyokuwa upande wa pili, kama unafurahia kupendwa basi na wewe kuwapenda wengine ni lazima, kwa maana wanahitaji hilo, na ni la kudumu.  Watu wanapata vidonda vya tumbo, presha na msongo wa mawazo na wengine afya zao kuzorota mara wakigundua hawapendwi au kutothaminika na watu walio karibuu nao. Ulishajiuliza siku mtu wako wa karibu akikutamkia ‘SIKUPENDI WEWE, YANI NATAMANI KAMA NISINGEIONA HIYO SURA YAKO’ utajisikiaje? Wakati fulani sio lazima mtu atamke, lakini mambo yake tu yanatoa picha kuwa hampendi mtu fulani.


Na wapo wengine wako katikati (neutral), yani yeye anajipenda yeye mwenyewe tu, mweee jamani, sasa si uende baharini huko utafute kisiwa ukae huko peke yako? Kama unaona hilo ni gumu, tafsiri yake ni kwamba tunahitajiana na kutegemeana. Unapotembea tu huko nje na kuona watu wamefurahi, hawana huzuni, hiyo ni dawa pia na fundisho kuwa huwezi kujifurahisha mwenyewe, ili mtu ucheke, lazima uchekeshwe na mtu mwingine, kama sio mko uso kwa uso basi hata kwa message tu mnazochati. Kwa lugha rahisi tujifunze kuwapenda watu pasi na kujali matabaka ya aina fulani

Angalizo: Kwakuwa kupendwa ni hitaji, wapo wanaotumia mgongo wa uhitaji huo na kupeleka kwa watu upendo nusu kilo,  mateso na maumivu kilo hamsini. Hiyo ni dhambi kwa maana mpokeaji alijiandaa kuwa aliyemuendea ni mtu mwema anayefahamu kuwa kupenda na kupendwa ni lazima kati ya mtu na mtu au jamii na jamii.
Ni rahisi kutamka neno NAKUPENDA, lakini ukweli tunao wenyewe mioyoni


KUPENDA KAMA AMRI
Upendo ni amri ya Mungu. Nimejaribu kufuatilia mawaidha ya dini zote, mathalani Wakristu na Waislamu, wote wameagizwa kupenda, na kwamba kama wasipowapenda binadamu wenzao basi na Mungu hatawapenda wao. Ahaaaaa, kumbe kama hujui kupenda basi huwezi kuambatana na baraka za Mungu. Upendo hauhitaji pesa au mazingira maalumu au kuwekewa mikakati kama bajeti ya kujenga reli ya standard gauge, la hasha! Ukitambua tu kuwa ni amri ya Mungu , basi ni kujifunza tu kuwa ni sehemu ya maisha yako.


Upendo unaozungumzwa hapa hauna masharti, vionjo tatanishi na vitenzi vichokozi vyenye mlengo wa kumuinua shetani. Kwani hujawahi kuona mtu anasema ‘nilimuua mume wangu ili niishi kwa amani na mtu NINAYEMPENDA’, Sasa huo ni upendo? Hapana, ni ushetani kwa maana huyu wasasa akibadilika kidogo tu na akaja anayejali zaidi, basi atamuua na huyu ili afurahie na huyo mwingine. Hivyo ndugu zangu ni bora tukafahamu jambo hili kinagaubaga ili tusichanganye mambo na kudhani kupenda ni hiari, hapana. KUPENDA NI LAZIMA, lakini KUHUSIANA NI HIARI YA MTU. Kumpenda mtu sio lazima muhusiane, au kuzoeana bila mipaka, hapana, tupendane, tushirikiane, lakini mipaka na heshima iwepo ili kulinda utu wa mtu, misingi ya kijinsia, utamaduni na uhuru wa kuamua juu ya msatakabali wa maisha ya baadaye ya mtu binafsi. Kama una swali, hoja au maoni, kuwa huru hapo chini eneo la comments. NAWAPENDA WOTE

Eng Nguki Herman. M
Instagram: @eng.ngukiwamalekela
Twitter: @engngukiherman
Asante kwa kupitia na kusoma haya.Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com

Thursday, 17 August 2017

ASIYETAMBUA NAFASI YA BIKRA MARIA KTK UKOMBOZI SIO MKRISTU!

Bikira Maria mama wa Mungu, Utuombee

Tumsifu Yesu Kristu/Bwana Yesu asifiwe/Shaloom.  Nakusalimu ndugu yangu katika Kristu Yesu mwana wa Mungu ambaye kupitia yeye tumekuwa wamoja kwa namna fulani. Naomba kukuondoa hofu kama utakuwa ni mmoja kati ya waliokwanzika na kichwa cha somo hili, kwa maana utakuwa umejikwaza mwenyewe kwa kujikataa au kuenda kinyume na ukweli. Kuwa mpole na usome taratibu maelezo yangu , na kama una hoja au kitu cha kupinga basi utatiririka hapo chini kwenye eneo la ku-comment, namimi bila hiyana nitakuja kukuweka sawa.

KWANI BIKIRA MARIA NI NANI?
Biblia takatifu imedadavua na kukakavua kinagaubaga juu ya mama Maria, fungua  kwa muda wako Injili ya Luka kuanzia sura ya kwanza aya ya 26 na kuendelea. Kwa kifupi Bikira Maria ni mwanamke safi, aliyeteuliwa na Mungu ili kupitisha nafsi yake ya pili (Yesu Mwokozi), yani kuwa mzazi wa Yesu Kristu Mungu kweli na mtu kweli. Alijazwa neema, kutunzwa na kulindwa ili abaki bila doa hata kumbeba mkombozi tumboni mwake. 

  Kama hiyo haitoshi, hakuishia kumzaa tu mtoto Yesu na kumuacha akapambane na hali yake, NOOOOOOO, aliendelea kumlinda, kumtunza (kumbuka pale walipokuwa wanamtafuta roho juujuu Luka 2:43-52), usisahau pale walipomkimbiza mtoto kwenda Misri  ili asiuawe na Herode (Mathayo 2:12-21) mara anaambiwa maneno ya kumchoma moyo juu ya huyu mtoto (Luka 2:35) bado akaendelea naye hata katika safari ya mateso hadi msalabani (Yohana 19:26-27)

Mafundisho makuu manne (DOGMA) kuhusu Mama Maria
  1. Maria Mama wa Mungu
  2. Maria Bikira Daima
  3. Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili
  4. Maria Mpalizwa Mbinguni


Leo sitaki kuanza kuyachambua hayo mnne kwa maana kila moja tu laweza kuwa mada ya kujaza kurasa nyingi. Angalau moja tu, kama huamini kuwa Bikira Maria makazi yake ni Mbinguni , nenda kasome Ufunuo sura ya 12 kuanzia aya ya kwanza na kuendelea na uje na jina la mwanamke anayezungumzwa hapo.

Wapo baadhi ya watu bila aibu mbele za Mungu wanasema kwao Maria sio kitu, wao wanamuangalia Kristu pekee kwa maana hakukuwa na ulazima wa Mungu kumtumia Maria na angeweza kumtumia hata mwanamke yoyote. Hivyo Maria alishamaliza kazi yake na hana umhimu wowote kwao. Hii ni kufuru mbele za Mungu ambaye ndiye aliyemtakatifuza huyu mama ili awe chombo kitakatifu kilichombeba mkombozi. Tatizo ni mafundisho yaliyokaa kimfumo wa kuoteshwa na vionjo vyenye ukakasi na kuwarithisha watoto uvuguvugu kisa tu hutaki kutafakari.

Maswali machache ya kujiuliza
  1. Kama unaamini kuwa Yesu Kristu ni Mungu kweli, nafsi ya pili ya Mungu Baba aliyeshikamana pamoja na Roho Mtakatifu bila kutengana, mbona unapata kigugumizi kusema Maria ni Mama wa Mungu (Yesu)?
  2. Kama Maria alishamaliza kazi yake ya kumzaa Yesu,na sasa hana umhimu wowote, basi na Yesu alishamaliza kazi yake na sasa hana umhimu wowote?
  3. Kama hakukukuwa na upekee wa Maria na Mungu angeweza kumtumia mwanamke yoyote, kumbe pia hapakuwa na ulazima wa Mungu kumtumia Yesu kutukomboa na angemtumia mtu yoyote?


Najaribu kuwaza kwa sauti hasa ninapoona wengi wakifanya mrejeo kwa wateule wengi wa zamani katika Biblia kama Musa, Elia, Daudi na wengine, lakini likija suala la Bikira Maria mhhhh, hapo wanaona mapichapicha. Wengi ukiwadodosa wanajing’atang’ata tu na kuishia kusema yeye anaangalia wokovu tu ulioletwa na Yesu, hataki kujua kuwa huyu Yesu hadi kutujia kuna watu ambao Mungu aliamua kushirikiana nao kujimwilisha (incarnation) ili tumuone na kumpokea katika umbo la kibinadamu. Kazi ya Bikira Maria ilitabiriwa tangu agano la kale huko Isaya  7:14 na kuelezewa matokeo yake katika agano jipya.

Angalau siku hizi kuna baadhi ya watu wa madhehebu yasiyo ya Kikatoliki wameanza kustuka na kujua kuwa walikuwa wanafanya makosa kutomheshimu mama wa Mkombozi wao hivyo kwa mbaliiiii wameanza kumtaja taja na kumheshimu, japo kwasababu ya kukosa msaada wa mafundisho au kuogopa wachungaji wao, basi wanashindwa kupata mang’amuzi ya hali ya juu na kujizolea neema kutokana na maombezi ya Mama huyu kwa mwanaye Yesu. Wapo ambao taratibu wameanza kusali Sala ya Salamu Maria na hata Rozali japo wanakuwa waoga kutokana na upande waliopo kutopigia chapuo sala hizi zenye nguvu ya kimungu ndani yake. Yeye mwenyewe kasema 'vizazi vyote tutamuita mbarikiwa' (Luka 1:48), sasa asijejua hili ni kizazi cha sayari gani?
Bikira Maria, Mama wa Amani, Utuombee


KUABUDU Vs KUHESHIMU.
Anayepaswa kuabudiwa ni mmoja tu (Kumbukumbu la Torati 5:7), naye ni Mungu muumba mbingu na nchi. Kuna watu pia wanapata ukakasi na kuwalishaa watoto wao matango poli kwa kusema wakatoliki wanamuabudu Bikira Maria, la hasha! Sio kweli, wao wanamuheshimu tu, tena heshima hiyo hatujakurupuka tu kumpa, bali ni Mungu kwanza ndiye aliyemuheshimu na kumkinga na doa la aina yoyote ili afanyike chombo cha kubeba nafsi yake kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Sasa jamani kama Mungu mwenyewe kamheshimu na kumpandisha hivi, sisi ni akina nani hata tumdharau? Ndio maana nimesema mtu asiyetambua nafasi ya Bikira Maria katika kuletwa kwa ukombozi huyo sio Mkristo bali anaigiza kuwa Mkristo.  

Bikira Maria ameshatokea mara kadhaa duniani hapa na ushahidi wa wazi kabisa upo. Maeneo kama Fatima, Lurdi Ufaransa, Kibeho Rwanda n.k yanatoa fundisho kwa dunia juu ya kumheshimu huyu mama. Hakuna mtu aliyewahi kupinga matokeo haya kwa maana ni matokeo ya wazi kabisa ambapo ni Mungu yule yule aliyemteua awe mama wa mwokozi anathibitisha kuwa uteule wake u hai hata leo huko mbinguni na duniani.
Bikira Maria ,kikao cha hekima, Utuombee

Kama unavyopata ujasiri wa kumwambia binadamu mwenzako akuombee kwa Mungu, sasa nakushauri utumie nafasi hii adimu kumwambia Mama Bikira Maria ambaye yuko Mbinguni uso kwa uso na Mungu akuombee kwa Mungu na mwanaye Yesu Kristu naye atafanya hivyo. Wewe omba kwa imani na matokeo utayaona.

TUOMBE:

Ee Mungu mwema, Baba wa Mataifa yote, kwa wema wako uliamua kumteua Mama Bikira Maria awe mama wa Mkombozi wetu Yesu Kristu, tunakuomba uturehemu na kutusamehe pale tunapokengeuka na kudharau heshima hiyo kubwa uliyompa mama huyu. Tena tunaomba msamaha na kwa mwanaye Yesu Kristu ambaye kabla ya kushuka duniani alikuwa kashikamana nawe kama nafsi yako, hivyo alishiriki kumteua mama Bikira Maria ili atusamehe na kutustahilisha baraka zako. Tena tunaomba msamaha na kwa Roho Mtakatifu ambaye mara kadhaa tumejigamba kujazwa naye kumbe ni vionjo vya kibinadamu na viini macho, na ndani mwetu tumejaa maasi hata kumdharau mama wa mkombozi. Nawe Maria Mtakatifu mama wa Mungu, utuombee kwa Mungu ili sala zetu ambazo mara kadhaa zinakwamishwa na maovu yetu ziweze kupokelewa, nasi kwa unyenyekevu tunaahidi kukuheshimu na kuthamini kazi yako ya kushirikiana na Mungu kutuletea Yesu, Bwana na Mwokozi wetu. Tunaomba hayo kwa njia ya Yesu Kristu, anayeishi na kutawala  pamoja na Baba, Mungu daima na milele. Amina

Eng Nguki Herman. M
Instagram: @eng.ngukiwamalekela
Twitter: @engngukiherman
Asante kwa kusoma katika blog yangu.Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com


Thursday, 27 July 2017

NO FORGIVENESS, NO LOVE

Someone who cannot forgive, by default cannot love.

I find myself recalling the law of magnetism in physics subject during my time in secondary school even in my engineering courses. If the piece of magnet cannot attract the opposite side (unlike poles) of the other magnet (S&N), automatically it cannot repel the similar side (like poles) of the other magnet (S&S/ N&N). You know what? Someone who cannot forgive, by default cannot love.  I have purposely started with forgiveness because it is simple to say ‘I will love you in any situation’ but not ‘I will forgive you for any mistake’

My dear brothers and sisters, it’s better we understand this day time truth; in forgiveness there is love and in love there is forgiveness. They work together with similar properties but different names just like improper subsets. In simple logic, someone who can find it difficult to forgive, yet he/she says that he/she can love you, automatically it’s not true.

In love there if fear of God; that’s avoiding to cause pains to someone else, and when happens accidentally, by default it will be very easy to ask for forgiveness. Love and forgiveness cannot be separated. “We are told that people stay in love because of chemistry, or because they remain intrigued with each other, because of many kindnesses, because of luck. But part of it has got to be forgiveness and gratefulness. ” ― Ellen Goodman

Carol Davis (counsellor) says; Real love is total commitment with no separate parts or degrees and filled with harmony and joy. Hopefully, that feeling is reciprocated by someone.  Love cannot be taught. It is a natural expression coming from the heart or emotional makeup of the individual.   It is a gateway to connection with another human being, and if a person is a Christian, to God.
Forgiveness is a part of love. If a person is unforgiving, this is a block to love. The ultimate test of love is forgiveness. 

 When someone that a person loves hurts him, the response is the true record of that love; if there is true love here, the person will not hold a grudge (a strong feeling of anger and dislike for a person who you feel has treated you badly, which often lasts for a long time ) become resentful, or fill the heart with bitterness.  None of these responses connect with true love.  It blocks that emotion.  So what should the response be: to forgive.
The Oxford English Dictionary defines forgiveness as to grant free pardon and to give up all claim on account of an offense or debt. True forgiveness is doing the complete opposite of what the emotions tell a person to do.  'I will forgive you if…….' is not forgiveness.
Forgiveness to be real must be unconditional. It does not mean that the hurt that has been experienced is minimized.  Forgiveness cannot be earned, bought, or bargained.  It has to be absolute.

There are two hurtful situations that occur between people who love each other: a wound and a wrong. The wound does not require forgiveness.  It was unintentional and accidental.  Time and patience will take care of this situation.
The other situation though is a different story.  A wrong is when a person knows that what he is doing will hurt the other person and does it anyway. It is a moral dilemma that the person faces and fails. To wrong someone that a person loves requires forgiveness. Forgiveness is instant; but trust must be built over a long period of time. Forgiveness takes care of the damage done. It lets the person off the hook.  However, the true test of love will be how the person works to rebuild that loving relationship. 

Forgiveness may be the single most difficult act of love. It is the difference between forgetting and letting go. The brain never lets the person forget, but the heart will give forgiveness. Love and forgiveness walk hand in hand in a relationship.
If we really want to love we must learn how to forgive’-Mother Teresa

It’s where now Michael Ugulini (Educator) adds; Forgiveness is a manifestation of love. People who truly love each other, whether in a marital relationship, as friends, or as family members, as examples, will forgive one another because of their outgoing concern for each other. Forgiveness is one way of expressing love and commitment to another human being. Even though we may be upset, hurt, wronged, and/or angry, love provides us the capacity for forgiveness.

When we love someone, even though it may be difficult sometimes, we ultimately desire to forgive them for any perceived wrongs against us. If we do not ultimately wish to forgive someone we say we love, then we're fooling ourselves, and them, as we do not truly love them.
Not extending forgiveness is putting ourselves first, well ahead of the person we claim to love. We are seeking our own desires and are not taking into account theirs. We are acting selfish and are not willing to give them the benefit of the doubt - or another chance. If we love them, we will forgive them and try to set the relationship back on the right track.

Words like ‘I hate him/her, I will never forgive him/her’ are poisons which is going to kill yourself because they will lead to love malnutrition.  It is better you train your mind and soul to forgive, because it will automatically be a fertilizer to sustain your love to others. “Resentment is like drinking poison and then hoping it will kill your enemies.” ― Nelson Mandela


NOTE: To forgive someone doesn’t need him/her (who hurt you) to repeat explaining what he has done to you. The strong soul forgives even before being asked to do so.If we really want to love we must learn how to forgive’-Mother Teresa

Eng Nguki Herman. M
Instagram: @eng.ngukiwamalekela
Twitter: @engngukiherman
Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com (Also subscribe to YouTube Channels- 'Eng Herman Nguki' and 'WaterDropletTv' )

Wednesday, 5 July 2017

MBABE WA MBABE WANGU ALIPONIZUSHIA UONGO

Tuwafundishe watoto kusamehe, lakini tusiwape hofu.

Katika maisha ya ukuaji kuna vitu sio rahisi sana kuvisahau hata kama havina tija sana. Moja ya vitu ambayo nilikuwa naogopa sana ni kupigana. Sasa kuna jamaa mmoja wakati niko shule ya msingi alikuwa hakai mbali sana na nyumbani alifanikiwa kufahamu kuwa nina huo woga. Na kwa sababu hata familia yao ilikuwa juu kimaisha alikuwa na ujasiri wa ziada, na kama hiyo haitoshi alikuwa kanizidi madarasa kama matatu hivi (tulikuwa tunasoma shule moja ya msingi huko Idodi-Kitanewa) na umri kanizidi.

Lakini hivi vyote sio kisingizio kwa maana mbinu za kupigana zipo nyingi tu hata kama mtu kakuzidi nguvu, kwani kwenye Biblia Daudi alifanyeje kumpiga Goliath? Ndivyo ilivyo  ndugu yangu. Sasa huyu jamaa alikuwa akijisikia tu ananipiga, dah, ukizingatia hali yetu ya maisha ya nyumbani, nikawa najiona dhaifu sana kumfanya chochote huyu jamaa, tena mimi nilikuwa naishi na bibi yangu tu nyumbani.

Basi kila nikipigwa na yule jamaa, nikawa naenda kusema kwa bibi ili aliruhusu namimi nimgoliatishe huyu jamaa ambaye alitumia udhaifu wangu kunigeuza mimi ngoma yake ya mazoezi. Ajabu bibi alikuwa ananizuia na anaishia tu kusema ‘wewe muache tu , nitaenda kuwaambia wazazi wake wamuonye asirudie hiyo tabia’. Nikawa nayaelewa yale maneno, japo huyu jamaa aliendelea na tabia yake ya kunipiga akijisikia hasa mkienda kucheza mpira maeneo ya wazi au tukienda mtoni huko kuogelea kipindi cha maji mengi na kuchoma viazi ( vimbwegea).

Mnyonge ukibahatika kupokonyoka hapo, ni kutimua mbio hadi mafichoni huko.
Kiukweli pamoja na kwamba huyu jamaa alikuwa amenizidi mabavu kwa mfumo fulani, lakini laiti bibi angeniruhusu tu nijitutumue nitakavyoweza, hakika ningetafuta cha kufanya kama alivyofanya mwenzangu Daudi wa kwenye Biblia, hata kutumia mawe tu au manati (Kwa maana nilikuwa nayo na kokoto za kutosha muda wote). Ile hali ilikuwa inanichefua sana na kujikuta wakati fulani nawaka hasira na kuona kama bibi pia anaiogopa ile familia kwa maana mama yake mdogo yule jamaa ndio alikuwa balozi wa  mtaa. Dah, lakini kulikuwa na fundisho kubwa sana kwa bibi kunizuia kumrudi yule jamaa, maana alikuwa ananiambia sentensi moja tu ya kihehe; ‘umtesa neke twangule nongwa’, akimaanisha utamuumiza  na mwisho wa siku tutazua kesi.

Yule mbabe wangu alikuwa na kaka yake, ambaye kiukweli alikuwa mpole sana, japo alionekana na nguvu sana lakini hakuwa mgomvi kabisaa. Na wakati fulani betri zikigeukiana kwa huyu mbabe wangu, yule kaka yake alikuwa anananisaidia angalau nipate upenyo wa kufanya mazoezi ya kukimbia hadi nyumbani. Aisee, usiombe kuishi maisha ya unyonge na kujiona huwezi kufanya kitu. Kama ni mtoto ni afadhari sana uwe na akili za darasani, angalau unakuwa na watu wa kukuogopa kwenye kipengere hicho, hasa wale ambao ikitolewa kazi wanakuja uwashushie vitu, wenyewe wanasema ‘unawasovia’ hata kama hakuna hesabu humo. Hawa watakutetea siku ukibanwa na waonezi wako, na wakati mwingine unawashitakia ili wakawapige mkwala waonezi wako.

ZAMU YA MBABE KUKUMBANA NA DHAHAMA

Siku moja ilikuwa sikukuu, kama sijasahau sana ilikuwa kati ya Pasaka au Krismasi. Sasa pale kwao wakaweka mziki na watoto tukawa tunaserebuka pale. Nilikuwa nacheza kwa tahadhari sana maana nipo nyumbani kwa mbabe wangu, na likitokea la kutokea yule jamaa atakuja tu hata kunikanyaga kama kifaranga, wahehe tunaita kiswiya.
Ilikuwa siku ya kufurahi sana kucheza mziki,lakini kuna jamaa alikuwa ananinyima amani.
Wakati mambo yanaendelea ikatokea ugomvi kati ya yule mbabe wangu na kaka yake. Weee nikajivuta pembeni kabisa mnyonge mimi. Katika purukushani yule mkubwa akamtwanga kichwa cha mdomoni yule mbabe wangu na kufanikiwa kumng’oa jino la mbele, kisha nayeye kuumia kwenye paji la uso kwa kuchimbwa na jino. Dah, kwakuwa yule mbabe wangu ana asili ya ukorofi, watu waliokuwepo walimuacha pembeni hapo akilia na kuugulia maumivu, kisha wakachemsha maji haraka na kuanza kumkanda-kanda huyu kaka mtu aliyeumia paji la uso.

Kwakweli nilikuwa namuonea huruma pia yule kaka mtu, na sikumuonea huruma kabisa yule mbabe wangu ambaye alijipatia mwanya wa lazima siku ile baada ya kung’oka jino kwa kupigwa kichwa na kaka yake. Ni kwasababu niliwaza kuwa huenda huku kuumia kutampa kipindi cha mpito cha kuugulia maumivu hivyo kutopata muda wa kuninyanyasa au kukwaruzana naye. Maisha yaliendelea ambapo baada  ya muda fulani kupita yule jamaa aliendelea tu na ukorofi wake na bado bibi aliendelea kunisisitiza nimsamehe tu na kuna wakati kweli bibi alikwenda kuwaambia wazazi wake juu ya tabia ya kijana wao ya kuninyanyasa, ambapo wazazi wake walimkemea na kumuonya aache hiyo tabia. Yule kaka yake nilimuamini sana na kuona ni mtetezi wangu.


MBABE WA MBABE WANGU AKAJA KUZUA YAKE

Maisha yaliendelea na walimaliza shule wale ndugu wawili kwakuwa walikuwa darasa moja, kisha yule mkubwa kufanikiwa kujiunga na sekondari.
Tarehe 15/06/2005 ilikuwa siku ya gulio (mnada) kule kijijini kwetu. Hiyo siku nilikuwa na hela yangu elfu kumi (10,000/=). Ilikuwa ni pesa yangu kabisa kutokana na kazi fulani niliyofanya, ambapo nilitumia elfu moja kununua kitu fulani na ikabaki eflu tisa. Sasa katika uhifadhi wa ile elfu tisa na utoto kuchangia, ile hela iliyobaki waliniibia yote. Nililia sana, kwa maana ile hela ilikuwa kubwa sana kwangu. Basi nikawasimulia baadhi ya rafiki zangu juu ya ule mkasa nilioupata. Sasa yule kaka wa mbabe wangu ambaye nilikuwa namuamini sana nayeye alipata hizi habari kuwa nimeibiwa hela elfu tisa.

Katika hali ya kustaajabu na isiyo ya kawaida huyu jamaa niliyemuamini sana baada ya kupata zile taarifa alikwenda kwa wazazi wangu na kuongea uongo wa kiwango cha lami na unaofanana na uuaji kabisa. Alisema, nanukuu: ‘Herman alikuwa na hela leo na amechezea kamali za mnadani. Mimi nilikuwa naye wakati anaenda kucheza. Nilimkatalia sana kuwa hao watakutapeli hao, yeye akawa mbishi, nikamvuta mkono tuondoke pale, lakini yeye aling’aang’ania kucheza hadi hela ikaisha. Nyie subirieni tu atakuja huku analia hapa’

Duh, aisee, ukweli ni kwamba ile siku hatukuonana kabisa yule jamaa hata ile kawaida tu kusalimiana, lakini alikwenda kuupika uongo huo ambao kiukweli, dah inauma sana. Muda ukawadia wa mimi kurudi nyumbani, kama alivyosema yule jamaa, nilirudi navuja chozi na hela sina. Mama alikaa kimya ili anisikilize kwanza nini kimenikuta huko. Nikamuelekeza kuwa nimeibiwa na sijuwi nini kimetokea, mama akanipa pole, lakini akasema ‘mbona fulani kasema umecheza kamali na alikuzuia lakini wewe ukawa mbishi?’ Mh, jamani, mbona mimi hata sijaonana naye leo? Akanieleza maelezo yote aliyosema yule jamaa, kuna kitu kilinikaba shingoni kwa hasira kwa maana nilijikuta najiuliza, :

  • Alikuwa analenga nini kuongea uongo huu kwa wazazi wangu?
  • Je hii hela ingekuwa sio yangu na nimetumwa na wazazi kununua kitu fulani kwaajili ya familia angeniweka katika mazingira gani?
  • Je hii hela ingekuwa ya mtu hata asiye ndugu yangu labda aliniagiza nikamnunulie kitu fulani huko gulioni na akapelekewa uongo huu uliosukwa kwa ustadi mkubwa, angejisikiaje?

 
Nilijiuliza mengi bila kupata majibu
Nafsi yangu ilichafuka sana ghafla na nilijikuta kwa mara ya kwanza namchukia sana kwa maana alifanya jambo ambalo sikutegemea. Hasira zilinizidi na kujikuta nalia sana na wakati huo mama alinituliza na kuniambia nimsamehe tu, na nijifunze kuelewa kuwa wapo watu wa aina hiyo na nimapungufu yao, japo mtu unayewasikiliza kama ukichukua mamuzi ya haraka, unaweza kusababisha madhara makubwa kwa taarifa za uongo na badaye kujikuta unajutia maisha yako yote. Nikajikuta hata msaada wake kipindi ambacho nilikuwa naonewa na mdogo wake nausahau kabisa, kwa maana kafanya jambo la kuogofya kwa mdomo wake.

Sijawahi kumuuliza hata siku moja, na tangu ile siku tumeonana kama mara mbili au tatu pekee hasa baada ya yeye kuwa shule ya bweni na mimi kuhamia Iringa mjini  mwezi wa nane 2005,na kuanza sekondari 2006. Tangu kipindi hicho nilikaa kwa muda na baadaye kuwasamehe wote wawili japo kipindi cha nyuma bado kuna roho ilikuwa inanituma nimtafute ili aniambie nini kilimtuma kuupika uongo ule. Wote kwa sasa wanaishi maeneo tofauti tofauti na familia zao.

HITIMISHO

Ndugu zangu, hakuna mtu mkamilifu hapa duniani, sote ni dhaifu. Kitu cha msingi ni kutouendekeza huo udhaifu wako (kilema cha dhambi) ambao unaweza kuwa na madhara makubwa sana kwako binafsi, familia au watu wanaokuzunguka. Mfano ni mimi mtu niliyemuamini kupita kiasi akaja kudhihirisha udhaifu wake kwa namna tofauti, lakini hii haiondoi ukweli kuwa kuna mambo mazuri aliyofanya ikiwemo kunitetea kipindi cha nyuma. Hata yule mbabe wangu, lazima tu kuna eneo fulani anafanya vizuri hata kama mimi sikuona binafsi, huenda ni kwa mwingine. Kitu cha msingi ni kusaidiana, kurekebishana, na wewe unayeonywa kubali kubadilika kwa maana hujuwi lini utakutna na lipi. EPUKA UONGO NA UGOMVI KWA MAANA UNAWEZA KUSABABISHA KIFO CHA MWILI AU NAFSI KATIKA MAZINGIRA MADOGO SANA.

Naitwa Nguki, sijawahi kumpiga mtu zaidi ya mimi kupigwa mara kadhaa wakati niko shule ya msingi. Baada ya hapo (kuanzia sekodari) kwakweli ni mkwara tu wa maneno umenisaidia kuepuka mapigano , kutotilia maanane maneno chonganishi yenye uchochezi wa kupigana pia kuomba msamaha hata kama sijakosa mimi ili yaishe na kuepusha mapigano. Kiufupi sipendi hata kuona tu watu wanapigana na sina huo mpango kwakweli.

Eng Nguki Herman. M
Instagram: @eng.ngukiwamalekela
Twitter: @engngukiherman
Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com

Wednesday, 28 June 2017

MWANAUME, KUMUOMBA MSAMAHA MWANAMKE NI HESHIMA.

Mwanaume anayejitambua haoni shida kuomba msamaha

Salamu. Leo nataka nizungmze na wanaume wenzangu. Hivi karibuni niliandika tafakari fupi juu ya mapishi na wanawake. Japo sikuweka huku kwenye blog, kule kule kwenye facebook, instagram na watsup kila mtu alitoa mtazamo wake, hasa watsup uliibuka mjadala mkali kwenye baadhi ya makundi ambako nilishirikisha. Na kiukweli lengo langu halikuwa kumaanisha kuwa mapishi ni ndoa, bali ndoa ni composite function ambayo ndani yake kuna vitu vingi sana, na lengo ni kuweka vitu vingine vyote sawa (keeping other factors constant /CETERIS PERIBUS) na kuangalia athali za mke ambaye hapendi au ni mvivu kupika.

Wakati wa kuchangia mada hiyo, wapo waliosema mbona umewazungumzia wasichana pekee? Nikaahidi kuja na ugonjwa unaowasumbua wanaume wengi kama compensation, kwa maana lengo ni kujenga na sio kushushua au kuhukumu. Sasa nizungumze juu ya suala la wanaume kuona ugumu kuomba msamaha kwa wanawake pale wanapowakosea. Ni ukweli usiopingika wanaume wengi hudhani wao kuomba msamaha kwa wanawake ni kujishushia hadhi au kuonesha udhaifu. Wengi hujitutumua na kuishia kusema ‘POTEZEA TU, au VUNGA, au YAISHE au KAUSHA’. Sasa sijui nini kinakaushwa hapa, ni mishikaki au chipsi? Sijuwi mimi.

Kwa haraka mtu anaweza kudhani hii ni kwenye ndoa tu, lakini hata kwa vijana ambao hawajaoa, inaweza kutokea mkakwaruzana au kukwazana na msichana yoyote mnayesoma naye au rafiki wa kawaida ambapo wanaume wengi hupata ukakasi kutamka neno ‘nisamehe dada yangu, nisamehe rafiki yangu’. Huu ni ujinga, na ujasiri wa hasara kwa maana haijaandikwa kuwa wanawake tu ndio watakuwa wanakosea. Ni vyema wanaume kujifunza kuomba msamaha pale unapomkosea mwanamke yoyote ili isikupe shida hata ukiingia kwenye ndoa na kufanya kosa fulani kwa mkeo, kisha kuanza kuona ukakasi kuomba msamaha. Ukiulizwa kitu ambacho unajua kabisa umefanya kosa, unaanza kujitutumua kuonesha hasira na kutengeneza mazingira kuwa kwa wanaume ni kawaida kufanya hicho kitu, hapana, hiyo sio kweli.
Kuomba msamaha hakukupunguzii kitu. Kwani hujuwi kuwa umekosa ?

Kwa mwanaume kuomba msamaha kwa mwanamke hakupunguzi uanaume wako wala kukudisqualify kutoka kwenye nafasi uliyopo, bali ni tendo la kijasiri na ukomavu kifikra , kimtazamo na maamuzi. Ile amani anayopata mwanamke baada ya kuombwa msamaha ni baraka kwako. Halafu masikini ya Mungu wanawake hata hawaoni kazi kusamehe, hasa ukionesha kweli umeelewa kosa. Mara nyingi kwasababu ya kujiona dhaifu hujikuta wanasamehe hata bila kuombwa msamaha, sawa hili ni zuri sana kuwa nalo hata kwa wanaume, lakini wakiombwa msamaha  inakuwa jema zaidi.

Hata huko kwenye ndoa mara nyingi baadhi ya dada zetu walioingia huko wanatushirikisha, utasikia ‘Weee baba fulani hata akirudi usiku usijaribu kuuliza, atakuwashia moto hadi ujikute wewe ndio unaomba msamaha kwa kumuuliza, amesema wanaume huwa hawaulizwi’, mhhh, hii sio sifa njema, sasa kama mnajiita nyie ni mwili mmoja, halafu unasema usiulizwe, basi na wewe usimuulize kitu. Ni kweli mwanaume ni kichwa cha nyumba na hilo ni agizo la Mungu mwenyewe, sawa lakini ukimkosea mkeo au mwanamke yoyote ufahamu kuna ubinadamu, na nafsi yake inafukuta na kujikuta anawaza  mambo mengi ya ajabuajabu ambayo angekufanyia kama angekuwa na huo uwezo.

Ushauri wangu kwa wanaume wote tujifunze kuomba msamaha kwa jinsia zote, na sio kwa mwanaume mwenzako tu kisa umeona ana minguvu kuliko wewe kwamba akiamua anaweza kukugeuzia betri na umeme ukashindwa kuwaka? Mhhh, hapana. Kama ambavyo inakukereketa mtu aliyekukosea asipoomba msamaha, ndivyo ilivyo kwa wanawake ukiwakosea na ukatia mgomo kuomba msamaha eti unaogopa kujishushia heshima, nani kakudanganya? Wewe omba tu msamaha kwa unyenyekevu wote, utajiongezea heshima kwake na kujitofautisha na wengine wanaochukulia kila kitu generally bila kuwa na unique behaviours.
Mwingine akijipapatua weee anaamua kuandika kaujumbe kamsamaha na kuweka mezani. Teh,teh, sawa ni jambo jema, lakini jifunze kutamka kwa kinywa chako then suppliment na hayo maandishi mazuri.

Kwa upande wangu sioni shida kuomba msamaha endapo nitagundua nimemmkosea mtu wa jinsia yoyote kwa maana hainipunguzii kitu chochote zaidi ya kuniongezea tu reputability na kutowaza kuwa hivi ananifikiriaje nilipofanya kosa au kumkwaza bila kuomba msamaha. Wafundisheni watoto wakiume kujua umhimu wa kuomba msamaha kwa vinywa vyao kwa jinsia zote pale wanapofanya makosa kama ilivyo kwa watoto wa kike. Hapo tutakuwa tunajenga jamii inayojielewa na kuifanya jamii kukalika na kuwa na mapatano pasi na kuwa na ubabe na unyanyasaji kwa watu fulani. Mtu anayeomba msamaha akikosa yupo kwenye nafasi nzuri ya kushirikishwa mambo mengi mazuri kwa maana anazungukwa na watu wasio na kinyongo. Usiombe mwanamke akuchukie kisawasawa kisa ulimkwaza na kugoma kuomba msamaha weeee, huwa wanachefuka hao balaa tupu. Tuwapunguzie mizigo ya kuwaza mengi, tuwaombe msamaha kila tuwakoseapo. OMBA MSAMAHA KILA UKIFANYA KOSA BILA KUJALI NI KUBWA AU DOGO. Tafakari njema.

Eng Nguki Herman. M
Instagram: @eng.ngukiwamalekela
Twitter: @engngukiherman
Unaweza kusoma mada mbalimbali kwa kuchagua mwaka/mwezi kwenye eneo la chini (footer block) ambapo baada ya kusoma bofya neno older post na zitakuja nyingine na uendelee kwa mfumo huo kupata mada za awali ambazo hukubahatika kuzisoma.Au kama hauoni hilo neno bofya kwanza 'view the web version' ndipo utakuja mfumo utakaokuonesha neno older post kwa chini. Kwa elimu na ujuzi kuhusu maji, kilimo, udongo na mazingira tembelea blog: www.wadcotanzania.blogspot.com